
Mwanahabari wa Nigeria Atengeneza Filamu Kuhusu Vurugu za Uchaguzi Tanzania
Mwanahabari mchunguzi kutoka Nigeria, @DavidHundeyin, ametangaza kutengeneza filamu maalum ya uchunguzi kuhusu vurugu zilizotokea wakati wa uchaguzi mkuu wa Tanzania wa Oktoba 29, 2025.
Kwa mujibu wa taarifa iliyochapishwa na Graphic Online, filamu hiyo inaitwa What Happened on October 29? na inalenga kueleza kile mwandishi huyo anachodai kuwa ni ukweli uliojificha nyuma ya matukio ya vurugu yaliyotikisa Tanzania baada ya uchaguzi huo.
Hundeyin alisema amefanya uchunguzi wa muda mrefu uliodumu kwa miezi kadhaa, ukihusisha mahojiano na mashahidi, uchambuzi wa taarifa mbalimbali za vyombo vya habari pamoja na kupitia ripoti ya tume ya uchunguzi iliyoongozwa na Jaji Mkuu mstaafu Mohamed Chande Othman.
Akizungumza kuhusu filamu hiyo, Hundeyin alisema:
“Kilichotokea Tanzania tarehe 29 Oktoba 2025 si kile ambacho dunia iliambiwa.”
Alidai kuwa simulizi nyingi zilizosambazwa kimataifa kuhusu vurugu hizo hazikuonesha picha kamili ya tukio hilo. Kwa mujibu wake, vurugu hizo zilikuwa zimepangwa na kuratibiwa mapema, zikihusisha watu wa ndani pamoja na nguvu kutoka nje ya nchi.
“Filamu hii ni jaribio la kuwasilisha mtazamo wa Kiafrika kuhusu simulizi la Kiafrika,” alisema Hundeyin.
Kupitia ukurasa wake wa X (Twitter), Hundeyin pia alitangaza ratiba ya uzinduzi wa filamu hiyo katika miji mbalimbali barani Afrika kabla ya kutolewa rasmi mtandaoni.
Katika ujumbe wake aliandika:
“Filamu hiyo itaanza kuonyeshwa rasmi Mei 26 mjini Accra, Mei 29 mjini Dar es Salaam na Mei 31 mjini Nairobi kabla ya kutolewa rasmi duniani kupitia YouTube Juni 1.”
Hata hivyo, matukio ya uchaguzi wa Tanzania wa 2025 bado yanaendelea kuzua mjadala mkubwa kimataifa. Wakati baadhi ya ripoti zilidai kuwa kulikuwa na matumizi makubwa ya nguvu dhidi ya waandamanaji na ukiukwaji wa haki za binadamu, upande mwingine ulidai kuwa baadhi ya taarifa na picha zilizosambazwa mtandaoni zilikuwa za kupotosha au zilizotengenezwa kwa teknolojia ya AI.
Indonesia






