
Mwenyekiti wa Umoja wa Wamiliki na Waendesha Bodaboda Mkoa wa Mbeya, Aliko Fwanda, amemwaga ukweli mzito mbele ya waandishi wa habari kufuatia vurugu zilizotokea jana Juni 21 kwenye mkutano wa Mbunge wa Mbeya Mjini, Patrick Mwalunenge, akimtaka mbunge huyo kuacha kuingiza migogoro kwenye sekta hiyo.
Fwanda amefunguka kuwa umoja wa bodaboda mkoani humo umepitia vipindi vigumu sana vya nyuma vilivyogharimu maisha ya madereva wengi kabla ya kufikia utulivu wa sasa, na akashangazwa na hatua ya mbunge kukurupuka kuitisha vikao vya siri bila kufuata utaratibu, jambo linalohatarisha kuwagawa na kuwasingizia vijana kupanga vurugu.
"Inabidi mbunge zimfikie taarifa hizi kwamba kabla ya hapa, huu umoja wetu kuna muda tulikuwa tunauliwa, tunatekwa kama kuku yaani tunachinjwa shingo. Yeye saa hizi amekuta bodaboda wametulia hawana malumbano yoyote, anakuja anaingiza migogoro na kutugawanya kisiasa kwenye makundi. Sisi tunayajenga makundi haya kwa gharama kubwa," amesema Fwanda kwa uchungu.
Mwenyekiti huyo amefafanua kuwa hakuwatuma vijana kwenda kuvuruga mkutano huo, bali madereva wenyewe walikasirishwa na kitendo cha mbunge kuitisha kikao cha "kunizia" akiwa hayupo. Alibainisha kuwa mbunge alimpigia simu na kumwamuru afike, lakini yeye alimfahamisha kuwa hakuwa na taarifa rasmi na alikuwa njiani kuelekea msibani.
Fwanda ametoa wito kwa viongozi wa Serikali na wabunge kujifunza kuheshimu mifumo na uongozi uliopo. Amesisitiza kuwa kama Mbunge Mwalunenge ana nia ya dhati ya kusikiliza kero za sekta hiyo, anapaswa kuwasiliana na uongozi rasmi ili uitishe mkutano mkuu wa jiji zima utakaofanyika kwa amani na uwazi.
Indonesia






